Monday, December 10, 2012

FAMILIA 300 IRINGA ZAKOSA MAHALI PA KUISHI


Nyumba iliyobomoka kutokana na mvua iliyoambatana na upepo mkali.

 ZAIDI ya familia ya 300 katika Kijiji cha Migoli,  Iringa Vijijini,  hazina mahali pa kuishi kufuatia nyumba zao kubomoka na nyingine kuezuliwa kwa upepo ulioambatana na mvua kubwa.

Mvua hiyo iliyonyesha juzi, ilianza saa 8:00 mchana ikiambatana na upepo mkali uliosambaratisha nyumba 57.
Nyumba 38 miongoni mwa hizo, zimezuliwa na nyingine 19 zimebomoka.

Diwani wa kata hiyo, Husein Kiswili. alilithibitisha habari kuhusu tukio hilo na kwamba uharibifu huo umehusisha pia miundombinu ya umeme na barabara  katika eneo hilo.

““Hali ni mbaya sana, watu hawana makazi kwa sababu nyumba nyingine zimeanguka, umeme umekatika kwa sababu nguzo zimeangushwa,” alisema Kiswili.

Alisema mbali na nyumba za wananchi pia baadhi ya  vyumba vya madarasa  ya shule ya msingi, vimeezuliwa na hivyo kusababisha wanafunzi kukosa masomo.

Diwani huyo alisema wakazi wa kijiji hicho kwa sasa wanahitaji msaada wa haraka wa kibinadamu.

Mbunge wa Isimani, William Lukuvi, alisema ameagiza timu ya maafa ifanye tathmini kuhusu  hasara iliyowakumba wananchi hao, ili aifanyie kazi.

Lukuvi pia aliahidi kutoa mabati kwa ajili ya kuezeka vyumba vya madarasa vilivyoezuliwa na upepo huo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk Christine Ishengoma, alitoa kilo  750 zachakula ili kusaidiwa waathirika wa tukio hilo.

Pia aliwataka wananchi kuwa wavuliivu na kusaidiana katika kipindi hiki kigumu. Dk  Ishengoma alisema Serikali inafanya tathimini ili kujua kiwango cha hasara iliyopatikana kutokana na mvua hiyo.

No comments:

Post a Comment

AddThis

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...